WHO: Mwongozo mpya kusaidia kupunguza vifo vya watumiaji pikipiki | | Habari za UN
Hii leo shirika la Umoja wa Mataifa la afya ulimwenguni, WHO kwa kutambua majeraha ya kichwa ndio sababu inayoongoza vifo vya waendesha pikipiki duniani, limezindua mwongozo mpya utakaowezesha mamlaka kuongeza matumizi ya helmeti kwa waendeshaji na watumiaji wa pikipiki.
Mwongozo huo umepitishwa hii leo huko Mumbai nchini India kunakofanyika mkutano wa siku mbili wa kanda ya Asia kuhusu Usalama Barabarani Duniani ukijikita katika matumizi ya helmeti bora kwa ajili ya kupunguza vifo na majeraha.
WHO inasema mwongozo utasaidia mamlaka kutunga sheria, kanuni na hatua zinazotakiwa ili kuongeza usalama, ubora wa helmeti na hatimaye kuokoa maisha.
Taarifa ya WHO iliyochapishwa leo inasema matumizi ya helmeti zenye ubora hupunguza hatari ya vifo mara sita zaidi ilhali hatari ya ubongo kuathirika hupungua kwa hadi asilimia 74.
Ukosefu wa helmeti bora, salama na zenye gharama nafuu, vinatajwa kuwa sababu za watu kutotumia helmeti, halikdhalika ukosefu wa helmeti za watoto, kutokusimamiwa kwa sheria zilizoko na joto.
WHO inasema helmeti ambayo haijavaliwa na kufungwa vizuri huongeza pia hatari ya kifo na majeraha iwapo ajali itatokea.
Ingawa hivyo bado matumizi ya helmeti kwenye nchi nyingi za kipato cha chini na kati ni kidogo licha ya ongezeko la kasi la pikipiki.
Dkt. Matts-Ake Belin, kiongozi wa Muongo wa Umoja wa Mataifa wa usalama barabarani mwaka 2021 hadi 2030 anasema kwa kuwa pikipiki zinaongezeka kwa kasi kubwa kwenye nchi za kipato cha chini na cha kati, hatua za dharura zinahitajika kuondokana na vifo na majeraha katika miaka ijayo.
Dkt. Belin anasisitiza kuwa mamlaka lazima ziweke sheria, mifumo na hatua za kuchagiza uwepo na uvaaji wa helmeti bora na mwongozo uliozinduliwa leo umetaja viwango vya ubora.
Mwongozo utasaidia kuanzisha mfumo wa kuchagiza matumizi ya helmeti, ikiwemo sheria ya kimataifa kuhusu helmeti, viwango vya ubora, usimamizi wa sheria na elimu.
WHO inasema mfumo wa matumizi ya helmeti zenye ubora na salama umesaidia Norway na Sweden kupunguza kwa kiasi kikubwa vifo na majeraha yatokanayo na ajali za pikipiki.