Makundi yenye silaha DRC waweweke chini silaha zao: Keita | | Habari za UN
Mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo DRC Bintou Keita amesema kwamba mpango wa Umoja wa Mataifa nchini humo MONUSCO unasisitiza wito wa Antonio Guterres, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kwa makundi yenye silaha yanayoendesha operesheni zao DRC kuweka chini silaha zao mara moja na bila ya masharti yoyote. Mwandishi wetu wa Kinshasa Byobe Malenga na taarifa zaidi.
Bi Bintou Keita, Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu nchini DRC ametoa kauli hiyo wakati wa mkutano na waandishi wa habari wakati akitimisha ziara yake mwishoni mwa wiki katika majimbo matatu ya Mashariki mwa nchi ambapo amesema amehuzunishwa sana na hali ya wakimbizi wa ndani, “Nilikuja kuona kwa uhakika athari za kuzorota kwa hali ya usalama katika maisha ya mamia kwa maelfu ya watu walio katika mazingira magumu, wakiwemo wanawake na watoto. Nimetembelea maeneo ya Bushagara na Mugwera huko Kivu Kaskazini na Kisoge huko Ituri. Nimekutana na wanawake na wanaume walio katika dhiki lakini ambao bado wana matumaini. Wana nia moja tu ya kurejea kwa amani ili warudi majumbani kwao salama. Haya ni matakwa yetu ya pamoja.”
Keita amewataka waasi wa kundi la M23 kuheshimu mkataba wa mwisho wa mkutano mdogo wa kilele uliofanyika mjini Launda nchini Angola ambao unaowataka waasi hao kuondoka na kurejea katika nafasi yao ya awali kwenye Mlima Sabinyo kabla ya Jumanne ya Machi 7 mwaka huu bila masharti kabla ya kutaka mazungumzo yoyote na serikali ya DRC,
“Ninakaribisha hatua ya mpatanishi wa Umoja wa Afrika, Rais wa Angola Joao Lourenço, ambayo imefanya Ijumaa kutolewa ahadi ya M23 ya kusitisha mapigano mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo kuanzia Jumanne tarehe 7 Machi saa 12 Jioni. Ninatoa wito kwa vuguvugu hili la waasi wa M23 kuheshimu bila masharti au kusita, masharti ya tamko la Luanda la Novemba 23, ambalo linadai wajiondoe katika maeneo yanayokaliwa, kusitishwa kwa mapigano yote, kuwaondoa wapiganaji wao na kurudi katika eneo lao la awali kwenye Mlima Sabino “.
Wito huo unakuja wakati waasi wa M23 wakiteka vijiji kadhaa katika maeneo ya Masisi, Rutshuru na Nyiragongo, hali iliyosababisha zaidi ya watu 600,000 kuyahama makazi yao.